Makala Elekezi: Kiswahili na Umajumui wa Kiafrika

M. M. Mulokozi

Abstract


Mustakabali wa lugha ya Kiswahili duniani umefungamana na harakati za kisiasa za kusaka umoja/umajumui wa bara la Afrika. Harakati hizo, zilizoanzia katika Diaspora ya Watu Weusi huko Amerika katika karne ya 19, zikapamba moto wakati wa ukoloni (takriban 1900-1960), na kupoa kidogo (bila kuzimika kabisa) baada ya Uhuru (t.1960-leo), zingali zinaendelea. Tunaziona katika miundo na asasi za kiserikali za umoja na ushirikiano wa Waafrika (k.m. EAC, OAU, AU, SADC, COMESA, ECOWAS). Aidha, tunaziona katika maingiliano na mashirikiano ya Umma wa Waafrika kuanzia Misri hadi Afrika Kusini, na kuanzia Amerika hadi Ulaya na Visiwa vya Pasifiki. Tunaziona pia katika mwamko wa kizazi kipya cha Waafrika ambao, licha ya vikwazo vingi vya kitamaduni, kilugha, kimbari na kiimani wanavyokumbana navyo, bado wanajitambua na kujitambulisha kuwa Waafrika. Harakati hizo zimedumu kwa kuwa zimefungamana na suala la kuwapo kwa Mwafrika hapa duniani.

Wasilisho letu linahusu dhima ya lugha, hususani lugha ya Kiswahili, katika harakati hizo za kuelekea katika Umajumui wa Kiafrika. Hoja yetu ni kuwa lugha haikupewa uzito wa kutosha katika harakati za awali za kujenga Umajumui wa Kiafrika, na kwamba huko tuendako inabidi tutambue na kukubali kuwa ni vigumu kuwaunganisha watu “wasioongea,” kwamba siasa na uchumi peke yake havileti umoja na utambulisho bila kuwa na kiungo thabiti cha utamaduni na lugha. Tunaungana na watangulizi wetu (Wole Soyinka, Ayi Kwei Armah na wengine) kusisitiza kuwa Kiswahili ndicho kinafaa kuwa lugha ya Ukombozi, Umoja, Umajumui na hatimaye Muungano wa Afrika yote. Hivyo mustakabali wa Kiswahili duniani umefungamana na mustakabali wa harakati za Mwafrika za kujenga Umajumui wa Kiafrika.


Full Text:

PDF

Refbacks

  • There are currently no refbacks.