MCHANGO WA TAASISI YA TAALUMA ZA KISWAHILI (TATAKI) KATIKA KUKUZA NA KUENDELEZA UWANJA WA FASIHI YA KISWAHILI YA WATOTO NDANI NA NJE YA TANZANIA (2009-2016)

L. H. Bakize

Abstract


Mwaka 2009, TATAKI, kupitia Idara ya Fasihi, Mawasiliano na Uchapishaji, iliamua kuanzisha kozi ya Fasihi ya Watoto na Vijana (KF 203) baada ya kupata ushauri wa mwalimu ambaye alikuwa ameanza kufanya utafiti wa uzamivu kwenye uwanja wa fasihi ya watoto (Lyimo, 2014). Ilipofika mwaka 2010 kozi hii iliamuliwa iwe miongoni mwa kozi za Programu ya Shahada ya Kwanza katika Taaluma za Kiswahili (B.A. Kiswahili) kwa mwaka wa masomo 2010/2011. Kozi hii inalenga kuwapa wanafunzi maarifa na mbinu za kutambua, kuelewa, kuchambua na kuhakiki kazi za fasihi ya watoto na vijana kwa nadharia na vitendo. Kwa upande wa uchambuzi, kozi hii inawapa wanafunzi mbinu mbalimbali za uchambuzi na uhakiki wa fasihi ya watoto na vijana katika vitabu, vyombo vya habari, na vyombo vingine vya kidijitali (TATAKI, 2010a). Wakati kozi ya fasihi ya watoto na vijana inaanza, ilikuwa ni kozi kwa ajili ya wanafunzi wa B.A. Kiswahili. Hata hivyo mwaka 2012 ilifanywa kozi ya lazima kwa wanafunzi wote wanaosoma digrii ya Ualimu na wanaochukua somo la Kiswahili kama somo la kufundishia wanapokuwa katika semesta ya pili ya mwaka wa pili. Mpaka tunapoyakamilisha makala haya, kozi hiyo bado ni ya lazima kwa wanafunzi tuliowataja. Pia, ni kozi ya hitiari kwa wanafunzi wengine nje ya hao tuliowataja. Tangu kuanzishwa kwa kozi hiyo, kwa kukadiria, wanafunzi zaidi ya 4,000 waliosoma shahada ya Ualimu katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaama, wakisoma pia somo la Kiswahili, wameisoma. Aidha, makala 16 katika uwanja wa fasihi ya watoto yamechapishwa, tasnifu mbili zimeandikwa kwa kiwango cha Umahiri na tasnifu moja ya Uzamivu. Hivi leo, uwanja huo wa fasihi ya watoto umeanza kuchangamkiwa kwa kuwa sasa unakua kwa kasi kutokana na mahitaji ya kitaifa na kimataifa (Ngugi, 2015). Makala haya yanakusudia kutathmini mchango wa TATAKI katika kukuza na kuendeleza uwanja huu tangu mwaka 2009 mpaka 2016. Ili kufanikisha azma ya makala haya mkabala wa kihistoria utatumika katika kueleza hoja zetu.


Full Text:

PDF

Refbacks

  • There are currently no refbacks.