Athari za Mafunzo-Kazini: Mfano Halisi wa Walimu wa Kiswahili Katika Shule za Upili Garissa

Geoffrey Nyaega Mogere, Moses Wasike

Abstract


Utafiti huu ulichunguza athari za mafunzo-kazini kwa walimu wa Kiswahili wa shule za upili katika gatuzi dogo la Garissa. Ulilenga kuchunguza nafasi ya walimu kuhudhuria warsha na makongamano ya Kiswahili. Aidha tathmini ya utoshelevu wa warsha na makongamano hayo ilifanywa. Mtihani wa Kiswahili umeendelea kushuhudia matokeo duni licha ya juhudi kubwa zilizofanywa na zinazoendelea kufanywa na wakereketwa wa lugha ya Kiswahili katika kukikweza. Sababu nyingi zimeshughulikiwa na watafiti wa awali na kuhusishwa moja kwa moja na matokeo duni. Japo mafunzo-kazini yametajwa kwa tutusa na baadhi ya wataalamu kama Kobia na Ndiga (2013) na Mose etal (2012) watafiti hawafahamu kuwepo kwa utafiti ambao umezamia mafunzo-kazini na uhusiano wake na matokeo ya mitihani ya Kiswahili. Utafiti huu ulitumia mpango wa utafiti wa kimaelezo. Uliwahusisha wakuu wa somo la Kiswahili ambao ni walimu wa somo la Kiswahili 13 katika shule 13 na walimu wakuu 13 wa shule hizo katika gatuzi dogo la Garissa. Walimu walipewa hojaji iliyolenga vipengele vinne: maelezo ya kibinafsi ya mwalimu, changamoto anazokumbana nazo katika ufundishaji na ujifunzaji, ufahamu na mahudhurio ya warsha na makongamano ya Kiswahili na msaada wa mwalimu mkuu katika kukuza uwezo wa mwalimu wa Kiswahili. Mwongozo wa uchunzaji ulitumiwa kutathmini kuhusika kwa mwalimu mkuu katika kumkuza mwalimu, kufadhili mahudhurio ya warsha na makongamano na juhudi zake za maksuudi za kuendeleza utekelezaji wa mtalaa wa Kiswahili. Utafiti huu ulionyesha kuwa wapo walimu ambao hawajawahi kuhudhuria warsha na kongamano la Kiswahili. Walimu waliowahi kuhudhuria wamehudhuria warsha na makongamano machache mno. Isitoshe wengi wa walimu wakuu hawatambui umuhimu wa warsha na makongamano ya Kiswahili. Utafiti huu unapendekeza kuhusika kwa wadau mbalimbali katika kuzipa warsha na makongamo ya Kiswahili uzito ufaao. Umuhimu wa sera madhubuti ya mafunzo-kazini unapendekezwa kama hatua ya kuimarisha mustakabali na utoshelevu wa warsha na makongamano ya Kiswahili. Pana haja ya  kuwahamasisha walimu wakuu kuhusu dhima na umuhimu wa mafunzo-kazini.


Full Text:

PDF

Refbacks

  • There are currently no refbacks.